Jumanne, 16 Juni 2015

VIPENGELE VYA FANI KATIKA TAMTHILIYA YA KIVULI KINAISHI



Katika makala hii tumeanza kwa kueleza dhana ya fani kisha tukatazama maana ya tamthiliya kulingana na wanazuoni mbalimbali, kisha tukagusia chimbuko na maendeleo ya tamthiliya kwa kifupi na mwisho tumejadili vipengele mhimu vya fani katika tamthiliya ya Kivuli Kinaishi iliyoandikwa na Said Mohamed.
 Kwa kuanza na dhana ya fani.
Fani ni ufundi katika kuumba umbo la kazi ya fasihi kutokana na ubunifu wake. Fani hujuisha muundo, mtindo, matumiziya lugha wahusika na mandhari (www.mwanchi.co.tz/makala/vipengele mhimu vya uhakiki wa kazi ya fasihi).
Fani ni ufundi wa kisanaa anaoutumia msanii katika kazi yake. Ni ustadi au ubingwa au mbinu ambazo msanii wa kazi ya fasihi hutumia katika kuwasilisha ujumbe wake kwa hadhira yake.(Senkoro 1982:8)
Fani ni sanaa, ni jumla ya vipengele vya lugha vilivyowekwa katika mpangilio mahususi ili kutoa kwetu maana Fulani (Mulokozi na Kahigi 1978:53).
Kwa ujumla, fani ufundi au ujuzi wa kisanaa atumiao mwandishi au mtunzi wa fasihi katika kufikisha ujumbe kwa jamii/hadhira iliyokusudiwa. Fani ni kipengele pekee ambacho humtofautisha kati ya msanii mmoja na mwingine, mfano wa vipengele hivyo ni matumizi ya lugha, mtindo, muundo, mandhari, na hata ujuzi wa wahusika.
Tamthiliya ni mchezo wa kuigiza au utungo wa kisanaa ambacho huweka wazo Fulani katika matendo na mazungumzo (Nkwera h.t.chombez.blogsport.com/2013/11/tmthiliya.htm/?.m=1)
Tamthiliya ni utungo wa kisanaa ambao huweka wazo Fulani katika matendo na mazungumzo (Tuki 2004).
Tamthiliya ni utungo wa fasihi ambao hubuniwa, kwa kiasi kikubwa kwa lugha ya mazungumzo yenye kuzua na kuendeleza matukio ya hadithi ya utungo huo. Chanzo cha matukio ya hadithi ya tamthiliya mara nyingi hupatikana humohumo katika mazungumzo ya wahusika wake  (Mazrui na symbo 1992). Mlokozi (1996) anasema hadithi ya tamthiliya husonga mbele kwa njia ya vitendo na mazungumzo ya wahusika. Hivyo anaonyesha bila wahusika hata mazungumzo hayatakuwepo. (chombez.blogspot.com/2013-11-01-achieve).
Kwa ujumla, tamthiliya ni andiko la kiuigizaji linalotoa simulizi kwa kuonyesha maneno na matendo. Hii inamaana kwamba tamthiliya ni utanzu ambao hauna msisitizo wa kuigizwa jukwaani ukilinganisha na drama na pia tamthiliya lazima ikidhi vigezo vya kidrama kwasababu isipokidhi inakuwa chapwa yaani haina shauku. Vigezo vya kidrama ni kama vile muonekano dhahiri wa jukwaani, mwonekano dhahiri wa hisia, usikiaji wa ngoma, ishara na matendo, ushiriki wa moja kwa moja wa hadhira na usikiaji dhahiri wa sauti za binadamu, ndege au wanyama.
Fasihi ya majaribio au tamthiliya ya majaribio ni fasihi iliyo lenga kuleta upya katika fasihi ya Kiswahili. Watunzi wengi wa tamthiliya ya Kiswahili walikuwa wakitunga kazi zao kwa kuiga mbinu mbinu na kanuni za tamthiliya ya ulaya. Kuanzia miaka ya 1970 watunzi wa tamthiliya ya Kiswahili hawakuridhika na uigaji huo. Waliona kuwa kuna umuhimu wa waafrika kuwa naTamthiliya yao yenye kuchota mbinu zake kutokana na sanaa za jadi za kiafrika. Lengo kubwa lilikuwa nikufanya Tamthiliya ioane na utamaduni na mazingira ya kiafrika(Mlokozi 1996).
Kwa mjibu wa Senkoro (2011:62-63) anaeleza kuwa majaribio mengi yanayofanyika katika Fasihi ya Kiswahili yanaelekea kuwa yamechota kutoka katika fasihi simulizi ya Kiswahili.
Kwa ujumla, Tamthiliya ya majaribio ni aina ya Tamthiliya ambayo hutumia mbinu na taratibu ambazo hazijazoeleka katika kumbo la kawaida la Tamthiliya, hii inamaana kwamba vipengele mbalimbali vya fani na maudhui ambavyo vilichukuliwa kutoka katika fasihi simulizi vikaingizwa katika tamthiliya ya Kiswahili ya majaribio ili kuonyesha utofauti uliopo kati ya Tamthiliya ya kiafrika na kimagharibi.
Hapo mwanzo kabla ya kuibuka kwa Tamthiliya ya Kiswahili ya majaribio hapa kwetu Afrika kulikuwa aina tofauti za sanaa za maonyesho kama vile utambaji, ngoma, miviga na sherehe ambazo zilikuwa na sifa zifuatazo: Zilitungwa hapo hapo, hazikuandikwa, hazikuwa za biashara, zilifanywa kwenye duara, hadhira na watendaji walibadilishana nafasi na sanaa iliyokamilika haikuwa ya mtu mmoja bali ya jamii nzima.
Baada ya ujio wa tamthiliya za kimagharibi umbo lake lilitofautiana na sanaa za maonyesho za asili kwani zilikuwa na mambo yafuatayo: Maandishi, waigizaji, hadhira, ukumbi, jukwaa, matapo, mgawanyo dhahiri wa majukumu(kazi), zilikuwa za biasharana zilikuwa mali ya mtu mzima. Hivyo waandishi wengi wazawa walianza kuandika kazi zao za tamhiliya kwa kufuata kanuni za uandishi wa kiaristotle.
Kuanzia miaka 1970 watunzi wa tamhiliya ya Kiswahili hawakuridhika na uigaji wa tamthiliya za kimagharibi(kiaristotle). Hivyo waliona kuwa kuna umuhim wa waafrika kuwa na tamthiliya yao yenye kuchota mbinu zake kutoka katika sanaa za jadi za Kiafrika. Lengo kubwa ilikuwa ni kuifanya tamthiliya ioane na utamaduni na mazingira ya kiafrika.(Mulokozi 1996).
Kwa kutumia mifano kutoka katika Tamthiliya ya KIVULI KINAISHI ya Said Mohamed    vipengele mhimu vya kifani vinavyojitokeza katika tamthiliya ya Kiswahili ya majaribio ni kama vifuatavyo:
Mtindo, ni jumla ya mbinu au sifa zinazomwezesha msanii kuwasilisha ujumbe wake au kuelezea msanii anavyounda kazi yake(Wamitila 2003). Katika kipengele hiki cha mtindo wasanii wengi wa tamthiliya ya Kiswahili ya majaribio huchanganya tanzu mbalimbali za kisanna kama vile nyimbi, ushairi na hadithi. Mfano, katika  tamthiliya ya KIVULI KINAISHI iliyoandikwa na Said Mohamed imechanganya tanzu mbalimbali kama nyimbo na hadithi. Mfano katika onyesho la nne.(uk.31) mwandishi ametumia wimbo anasema;
“NYIMBO: Nasikia parakacha myembeni
    Kam mshambigija mleteni

            Eee wewe … eee wewe
  Kupeana ni kikoa,
     Toa name nitoe
       Ati kupeana ni kikoa
     Toa name n’toe!”
 Utanzu mwingine alioutumia katika Tamthiliya hii ni hadithi mfano katika onyesho la kwanza (Uk10) msanii anasema ;
                        “Bi.kizee;  Haya(anaingia hadhira huku anavuta ugoro na huku
                                           anapakasa ukili wake- kaketi kijamvini) paukwaa….
                          Wtoto na
                           hadhira:    kimya
                           Bi. Kizee:  paukwa…….
                           Watoto na
                           hadhira;    kimya
                           Bi. Kizee:  paukwa…itikieni….itikieni basi….
                           Watoto na
                           hadhira;     Pakawa….”
Kwa hiyo mbinu hii ya kuchanganya tanzu katika kazi moja ya fasihi husaidia hadhira kuvutiwa na kuhamasisha kwa wasomaji kutokana na kuoana na utamaduni wao.
Vilevile methali zimeweza kujitokeza katika( Uk.24) anasema,
“unachumia juani na kulia kivulini, (Uk.67) kikulacho kinguoni mwako, (Uk.111) majuto ni mjukuu, (Uk.6) kuishi  kwingi kuona mengi na kujua mengi pia”.

Muundo ni mpangilio wa kiiufundi anaoutumia msanii katika kazi yake(Senkoro F.E.M.K(1982). Kwa ujumla muundo ni mpangilio na mtiririko wa kazi ya fasihi simulizi kwa upande wa visa na matukio, muundo hujumuisha jinsi msanii wa kazi ya fasihi alivyofuma, alivyounda na anavyounganisha tukio moja na lingine, kitendo kimoja na kingine wazo na wazo, sura moja na nyingine, ubeti na ubeti, hata mstari wa ubeti na mwingine. Mfano katika tamthiliya hii ya KIVULI KINAISHI kuna visa viwili nadi ya kisa kimoja yaani kisa cha Bi kizee na watoto na kisa cha maisha ya Giningi. Vilevile mwandishi ametumia Mianzo na miishio ya kifomula mfano, mianzo ya kifomula(Uk10) msanii anasema:
                                 “Bi.kizee; Haya(anaingia hadhira huku anavuta ugoro na
                                                  huku anapakasa ukili wake- kaketi     kijamvini) paukwaa….
                                   Wtoto na
                                   hadhira:       kimya
                                   Bi. Kizee:    paukwa…….
                                   Watoto na
                                   hadhira;       kimya
                                   Bi. Kizee:    paukwa…itikieni….itikieni basi…
                                   Watoto na
                                   hadhira:      pakawa….”
Pia ametumia miisho ya kifomula mfano, ukurasa wa mwisho kabisa (Uk130) onyesho la 10 mwandishi anasema;
           “ Bi.kizee: Basi huo watoto ndio mwisho wa hadithi…na kama mwisho wa hadithi ulivyo
                           Huwa furaha au huzuni”
Kutokana na kipengele hiki cha mianzo na miisho ya kifomula katika Tamthiliya ya kiswahili majaribio kimeleta upekee kwa sababu huvuta umakini wa hadhira kuwa na shauku ya kutaka maudhui ya Tamthiliya, na hii ni kutokana na maneno anayotumia msanii katika kuanza kazi yake.
Matumizi ya lugha, ni namna ambayo msanii ameteua na kupangilia tamathali za sema kama sitiari,tashbiha, takriri, tashihisi, tafsida, methale, misemo, nahau, taswira na lugha za kigeni (Senkoro F.E.M.K 1982). Katika Tamthiliya ya “KIVULI KINAISHI” iliyoandikwa na Said Mohamed. Mwandishi ametumia taswira mbalimbali kama ifuatavyo: KIVULI KINAISHI ni taswira inayo maanisha mawazo ya kimpinduzi yaliyokwisha pandikizwa na kwa vizazi vipya ili kudai haki na usawa. Taswira nyingine ni “unga wa rutuba” (uk112) yenye maana ya elimu ya kujitambua katika jamii na kutambua nafasi yako na kuwa na uwezo wa kuwaelimisha wengine.
”Bi.kirembwe: Enh! (anashituka….anashangaa) umebwia nini?
  Mtolewa: unga wa rutuba…..
   Bi.kirembwe: unga wa rutuba……a-a-a-a-a-mbaya…..mbaya
   Mtolewa: Ndiyo…………”
Taswira nyingine ni “unga wa ndere” wenye maana ya itikadi zinazomfanya mtu katika tabaka tawala akubalike na kushika miiko mfano (Uk.111) Mtolewa anasema:
           “Mtolewa: Mtolewa wa leo hayupo pamoja na wewe … yuko
                             maili elfu na moja mbali na wewe. Mtolewa wa
                              leo hasimamii mamlaka uliyompa, anasimamia
                              mamlaka ya hawa wote   waliopewa unga wa ndere..”
 Taswira nyingine ni mdundo wa ngoma unaomaanisha kitendo cha kufuata mashariti kama tabaka tawala litakavyo (Uk.31) katika onyesho la nne.
                                   “Kumbwaya, ugoma maarufu wa Giningi, analia, kabla
                                     pazia kufunguliwa.Nyimbo nyimbo inakuja na ngoma inaimbwa
                                     kwa sauti za kike kwa kiume, za wakubwa kwa wadogo:
                                     Pazia linafunguliwa kidogokidogo kuwaridhisha wari
                                     Wanaotaka kuingizwa giningi.”
vilevile mwandishi ametumia takriri katika onyesho la nane (uk.111) anasema,
          Bi.kirembwe: “Ulumbi …ulumbi… uluumbi (anakwenda huku akirudi huku)
                                 Umechomoka Mtolewa, majuto hakika ni mjukuu
                                  nilihisi mimi tokea mwanzo,lakini sijui kanini sikuchukua hatua?”
Hivyo kipengele hiki cha lugha  katika Tamthiliya za kimajaribio kimeweza kuleta upya katika kazi za fasihi kwa kuingiza vionjo asili vya kiutamaduni na  kuepusha migogoro ya moja kwa moja kati wasanii na tabaka tawala kwa kutumia lugha ya mficho kwa kutumia taswira.
Wahusika, ni binadam wanaopatikana katika kazi ya fasihi ambao wana sifa za kimaadili, tabia, kiitikadi na falsafa ambazo hutambulishwa na wanayoyasema na wanayoyatenda.(Wamitila 2002). Katika tamthiliya wahusika hujidhihirisha katika utambaji mfano, katika Tamthiliya ya KIVULI KINAISHI iliyoandikwa na Said Mohamed amefanikiwa kwa kiasi kikubwa kuwashirikisha hadhira katika utambaji. Mfano (Uk.60) onyesho la tano mwandishi anasema:
Mtangazaji: Mpo? Wali mpo?
Wali wote: tupooo!
Mtangazaji: yote sawaaa?
Wali wote: yote sawa…sawa….sawa…
Vilevile amefanikisha kuwashirikisha hadhira (Uk10) msanii anasema,
             Bi. Kizee:  paukwa            
             Watoto na
             Hadhira:  Pakawa….
Hivyo basi ushirikishwaji wa hadhira ni muhimu kwa sababu huipa Tamthiliya uhai, mvuto na kuondoa uchovu kwa hadhira.
Mandhari, ni sehemu ambayo matukio ya hadithi au masimulizi hutokea.mandhari huweza kuwa halisi kama vile njiani, msituni, kijini mjini au ya kufikirika kama vile kuzimu, peponi na mbinguni(Senkolo F.EM.K.1982). Vilevile mandhari ni elementi ambayo hutufichulia wapi na lini ambapo matukio Fulani yalifanyika(Wamitila 2002).mwandishi anaweza kutumia mandhari halisi nay a kuonekana au mandhari ya kufikirika. Mfano katika tamthiliya ya KIVULI KINAISHI mwandishi ametumia mandhari halisi ya kitanzania kutokana na kutaja kwa miji kama vile unguja na pemba vile vile mambo kama rushwa, uongozi mbaya na hali ngumu ya maisha vinaashiria nchi za dunia ya tatu kama vile Tanzania ambapo baadhi ya viongozi hutumia madaraka yao vibaya. Vilevile kuna mandhari ya kubuni katika onyesho la tisa (uk.117)mwandishi anasema,
“BI KIREMBWE: Na sauti hiyo inatoka wapi?
SAUTI: Kuzimu…..
BI KIREMBWE: Aha, sasa naanza kuelewa… sauti hiyo ni sauti ya Mtolewa 
                             inayotoka  kuzimu...”
Hivyo mandhari huifanya kazi ya fasihi kuendana na uhalisia hasa mandhari halisi.
Kwa ujumla vipengele hivi ndivyo hutofautisha Tamthiliya ya Kiswahili ya majaribio na kuipa upekee ukilinganisha na Tamthiliya zilizotungwa kabla ya miaka 1970s ambazo zilikuwa na mlengo wa Tamtiliya ya kimagharibi ambapo watunzi wa Tamthiliya hawakurithika na uigaji huo, wakaona kunaumhimu wa waafrika kuwa na Tamthiliya yao yenye kuchota mbinu zake kutokana na sanaa za jadi za kiafrika.
            

                          


MAREJELEO
Faustine, S. (2015) Tamthiliya ya Kiswahili Chuo Kikuu cha Dodoma:  (Hakijachapishwa.)
Mohamed, S. (2009) Kivuli Kinaishi: Oxford University Press, East Africa ltd. Nairobi.
Mlokozi, M.M (1996) Fasihi ya Kiswahili: Taasis ya Uchunguzi wa Kiswahili; Chuo Kikuu cha Dar- es- Salaam.
nkwerah.t.chombozi.blogspot.com.n/2013/11/tamthiliya.htm/?.m=1
Nyangwine, N.& Masebo, J( 2007) Fasihi kwa ujumla. Nyambari Nyangwine Publisher: Dar- es-Salaam.
TUKI (2004) Kamusi ya Kiswahili Sanifu: Chuo Kikuu cha Dar-es- Salaam.
www.mwananchi.co.tz/makala/vipengele muhimu vya uhakiki wa kazi ya fasihi.
Senkoro, F.E.M.K (2011) Fasihi Dar- es- Salaam University Press: Dar- es- Salaam. 












DHANA YA KAMUSI NA MAUMBO NUKUZI YAKE



 Dhana ya kamusi imejadiliwa na wataalamu mbalimbali, na zimejibainisha kama ifuatavvyo;
TUKI ( 2004) wanaeleza, kamusi ni kitabu cha maneno yaliopangwa kwa utaratibu wa alfabeti na kutolewa maana kwa maelezo mengine.
Zgusta akinukuliwa na Mdee anaeleza, kamusi ni kitabu cha marerejeleo chenye msamiati ulio kusanywa kutoka kwa wazungumzaji wa jamii fulani na kupangwa katika utaratibu maalumu, kisha kufafanuliwa kwa namna ambayo wasomaji wanaweza kuelewa.
OXFORD  (2010)  wanaeleza kuwa kamusi ni kitabu ambacho kina orodha ya maneno ya lugha fulani katika mpangilio wa alfabeti na huelezwa maana ya maneno hayo. Pia  kamusi ni orodha ya maneno yaliopo katika mfumo wa kielektroniki mfano yanaweza kuhifadhiwa katika komputa.
Kwa ujumla kamusi ni kitabu kilichobeba orodha ya maneno mbalimbali ya lugha fulani yaliopangwa katika mpangilio wa kialfabeti na kutolewa maana zake kwa namna ambayo wasomaji wanaweza kuelewa.
Katika kueleza dhana ya maumbo nukuzi Abel  John, (2012) mwanafunzi wa chuo kikuu cha Dar Es Slaam katika makala ya Kiswahili anaeleza kuwa maumbo nukuzi  ni umbo la msingi la neno, mfano;  maneno lima, cheza, kula, imba na soma.
 Kwa ujumla, maumbo nukuzi ni umbo la msingi la neno linaloingizwa katika kamusi na kusimama kama kidahizo katika kamusi, hivyo maneno kama vile imba, lima na cheza ni maumbo msingi ya maneno yaingizwayo katika kamusi, mathalani husimama katika vidahizo.
Maumbo nukuzi yapatikanayo katika kamusi ni kama vile:
Maumbo sahili, Haya ni maneno huru yasiyo na utegemezi  au yasiyo na utegemezi, mfano; baba, mama, barua, bakuli, nyumba na cheza, haya ni maumbo huru yasiyo na utegemezi na huingizwa katika kamusi kama vidahizo.
Maumbo ambatani, Haya ni maneno ambayo huumbwa kwa kuunganishwa maneno mawili tofauti kama vile nomino na kitenzi, nomino na nomino na maneno mengine. Katika  kamusi maneno haya huchukuliwa kama neno moja lenye kuwakilisha dhana fulani. Maumbo haya yamejitokeza katika kamusi ya TUKI [2001] kama vile:
                    Kipaza+sauti                 kipazasauti
                   Kipasha+moto                kipashamoto
                   Kipima+hewa                 kimahewa
Maneno haya yote ni mwambatano lakini husimama kama neno moja katika kamusi na katika kamusi hatuangalii neno moja moja bali hata misemo na nahau ambayo pia huchukuliwa kama neno moja lenye kuwakilisha dhana fulani. Mfano  TUKI(2001) wametoa mifano kama vile:
                Kifungua +kinywa                    kifunguakinywa
               Tia+nanga                                 tiananga
               Piga+maji                                  pigamaji
Licha ya maneno haya kuwa yana uambatani wa zaidi ya neno moja, hutoa maana moja yenye kueleza dhana fulani inayobebwa na maneno haya.
Maumbo hulutishi, haya ni maumbo ya maneno ambayo hutokea kama kidahizo katika kamusi, maneno haya huuundwa kwa kuunganisha sehemu mbili za maneno tofauti na sio sehemu nzima. Oxford (2010)  wametoa mifano kama vile:
Telephone
Mobitel                               mobile telephone
Telefax
Maneno haya ni sehemu ya maneno fulani ambayo husimama kama kidahizo na kutoa maana iwakilishwayo na maneno hayo yaliyo hulutishwa.
Maumbo ya Akronimia, haya ni maumbo ambayo huingizwa katika kamusi kama kidahizo na huwa na ufupisho ambao huwakilishwa kwa herufi kubwa ambapo kila herufi hubeba maana fulani. Kamusi  ya Oxford (2006) imetoa mifano kama vile:
           ISBN                                     International Standard Book Number.
           ISDN                                   International Granted service Digital Network.
Akronimia hizi hutokea upande wa kidahizo kuwakilisha maana au dhana iliyo ndefu kuwa katika maneno machache.
Maumbo rejezi, Haya ni maumbo ya kumfanya msomaji arejee ili kupata ufafanuzi zaidi. Katika  kamusi huoneshwa kwa kutumia alama ya mshale ambao hulenga kumuonesha msomaji kulitafuta neno linalooneshwa ambalo lina uhusiano na kidahizo kinachoshughulikiwa na msomaji, iliawze kupata uelewa wa kina juu ya kidahizo hicho.
Mfano TUKI (2010) Wameonesha urejezi kama vile
               Pas.try                      see also
               pipe                           see also pin pipes
Mshale huu huwekwa baada ya taarifa ya kidahizo husika ili kumfanya msomaji aweze kurejea kidahizo fananifu na kinafanana na kile kinachoshughulikiwa na msomaji.
Maumbo dondoshi, Ni maumbo ambayo huingizwa katika kamusi kama kidahizo baada ya sehemu ya neno hilo kudondoshwa. Mfano Oxford (2010) wametoa mifano kama vile:
               Phone from telephone
              Gram from telegram
             Bike from bicycle.
Maumbo haya hubeba maaana ambayo hupatikana katika neno zima kabla hata halijafupishwa.
Maumbo radidi, Ni maumbo ya neno linalojirudia katika kamusi na neno hilo hubeba dhana moja katika kamusi.
       Mifano: -   urambembe
       -   Myungiyungi

Maumbo haya hubeba dhana moja inayowakilishwa na uradidi huo.
Maumbo ya homonimia, Ni maumbo ambayo huwa sawa katika maandishi, matamshi lakini huwa tofauti katika maana za maneno hayo, katika kamusi maneno haya hutofautishwa  kwa kupewa namba, mfano,
Kaa1
Kaa2
Kaa3
Na tofauti ya maneno  haya yanaonekana katika kitomeo, yaani maelezo yatakayotolewa kuhusiana na kidahizo hicho.
 Kando na maumbo nukuzi, kamusi pia ina matatizo yake, nayo ni kama yafuatayo;
Upotezaji wa uasili wa asili ya kidahizo husika. Katika  uandaaji wa kamusi kuna baadhi ya maneno hupoteza uasili wake pindi yanapoandikwa na kuingizwa kama vidahizo. Mfano maneno kama;
                    Kusoma                                   soma
                   Kuimba                                     imba
                   Kucheza                                    cheza
Kutokana na tatizo hili inashauriwa kuingiza vidahizo katika myambuliko na kuweka utangulizi unaoeleza kuwa umeingiza vitenzi kutokana na mzizi. Mfano,
                   Kucheza, chezea, chezesha na  chezeka yameingizwa kutokana na mzizi ‘ chez’
                  ambayo husimama kama kidahizo ‘cheza’.
Tatizo lingine ni utofauti wa matamshi wa lahaja moja ambayo huwa vigumu kuweka vibadala vyote. Mfano,
                  Bomba la maji- watu wa bara huita bomba
                                          -watu wa pwani huita kifereji
Hii hupelekea mtunzi wa kamusi kupata shida katika kufafanua dhana hii kwa kuwa na lahaja zaidi ya moja. Kutokana na tatizo hili inashauriwa kuchagua vidahizo katika lahaja moja na kuweka utangulizi  unaotolea ufafanuzi juu ya lahaja iliyoandikiwa sana.
 Tatizo la mwisho ni kupanga vidahizo kialfabeti. Hili pia ni tatizo kwani wanalugha wanafahamu  maneno ya lugha kiasili yake, hawafahamu isimu na maneno magumu kupanga kialfabeti. Mfano ,
                          Kucheza  kuwa cheza 
                          Kupika  kuwa  pika
Maneno yote haya hutafutwa katika kamusi kwa kufuata mpangilio wa kialphabeti. Hii husababisha wanalugha kushindwa kutafuta maneno  wanayohitaji kupata dhana zake. Kutokana na tatizo hili inashauriwa kuweka utangulizi mzuri utakaoonesha mpangilio wa alfabeti  zilizotumika katika uwekaji wa vidahizo hivyo ili iwe rahisi kwa mwanalugha yeyote kutafuta dhana ya neno aliolikusudia kwa haraka. Mfano,   Kamusi ya Kiswahili ya F. Johnson (1962-vi ) anatolea maelezo juu ya utangulizi wake kama ifuatavyo;
                       Maneno yamepangwa kufuata taratibu ya alfabeti, yaani a, b, ch, d, e, f, g, h, I, j,
                      k, l, m, n,  o, p, r, s, t, u, v, w, y, z.
Pia anaendelea kutoa ufafanuzi katika (viii) anasema,
                    kwa ajili ya watu wasiojua Kiswahili sana, tumeonyesha namna ya kufanya maneno
                   ya wingi ya majina hivi. Kitabu, vi-; pipa, ma-; mtu, wa-; ulimi (ndimi); nk; yaani
                  neno la wingi la kitabu ni vitabu, la pipa ni mapipa, la mtu ni watu, la ulimi ni ndimi.
                 Majina yote yamepigwa chapa kuanzia herufi kubwa.
Kwa ujumla kumusi husaidia kwa kiasi kikubwa kukuza lugha kutokana na wanalugha kupata dhana  za maneno mbalimbali kutoka kwenye kamusi na kuyatumia. Hii husaidia misamiti mbalimbali kutumika kwa kiasi kikubwa na kuenea ua kusambaa kwa wanalugha wengi, ambayo hupelekea kukua na kuenea kwa lugha kwa ujumla.


MAREJELEO.
F. Johnson (1962), Kamusi ya Kiswahili. The Sheldon Press: London.
Oxford (2010), Oxford Advanced Learners  Dictionary. Oxford  University Press: New York.
TUKI (2004), Kamusi  ya Kiswahili Sanifu. TUKI: Dar es esaalam.
                                

 TANBIHI: Kwa makosa ya kitahajia na kimaana yanayoweza kujitokeza kwenye kazi hii nia makosa  ya kiuchapaji hayahusiani na vyanzo rejewa vilivyotumika.